Monday, April 17, 2017

Mkwasa ameelezea ‘picha’ la wachezaji wa Yanga kuachwa na ndege Algeria

Baada ya kuchapwa 4-0 na kuondoshwa kwenye michuano ya kombe la shirikisho Afrika, klabu ya Yanga ilipata pigo jingine kufuatia baadhi ya wachezaji pamoja na katibu mkuu Charles Boniface Mkwasa kuachwa na ndege baada ya kuchelewa kufika uwanja wa ndege.
Yanga walijikuta wameachwa na ndege baada ya kuchelewa kuripoti kwenye uwanja wa ndege kwa ajili ya kukaguliwa kabla ya safari, kundi la wachezaji 11 pamoja na Mkwasa walitakiwa kusafiri kwa ndege ya mchana lakini walifika uwanja wa ndege na kukuta ndege waliyotakiwa kusafiri nayo imeshaondoka.
Wachezaji wengine walifanikiwa kusafiri lakini ni wale waliotakiwa kuondoka kwa ndege ya jioni, Yanga walikwenda Algeria kwa makundi baada ya kushindwa kupata tiketi za pamoja kama timu, hivyo hata kurudi walipaswa kusafiri kama walivyokwenda.
Mkwasa ameelezea mkasa mzima wa tukio la kuachwa na ndege huku uhakika kurejea Tanzania ni hadi April 20, 2017.
“Baada ya kurudi kutoka kwenye mechi, tulipofika hotelini nilitanganza kwamba, kundi la wachezaji watakaoondoka mchana basi waondoke asubuhi baada ya chai (saa 2) waende uwanja wa ndege na kundi ambalo litaondoka mchana basi waondoke saa tano kwenda uwanja wa ndege.”
“Watu wakasema tutakaa sana uwanja wa ndege kwa hiyo bila kuangalia tiketi wakasema tuondoke saa tano kwenda uwanja wa ndege. Ilipofika saa nne tukaondoka kwenda uwanja wa ndege, kutoka tulipofikia hadi uwanja wa ndege ni parefu kidogo, tulipofika pale tukakuta milango imeshafungwa na ndege imeondoka na hakuna ndege yoyote.”
“Ndege iliyokuwepo ilikuwa tayari imeshajaa, na usafiri utakuwepo kuanzia tarehe 20, kwa kuwa na sisi tulisafiri kiutu uzima ikabidi turudi hotelini tuwapumzishe wachezaji tuwatafutie mahali pa kula na tunajaribu kufanya mawasiliano na wenzetu tuliocheza nao (MC Alger) kuangalia ni jinsi gani tunaweza kuishi lakini kiujumla ni kwamba hiyo ndio hali halisi ilivyokua.”
“Niseme tu kwamba, baada ya kutoka kwenye mechi watu wakawa wamechanganyikiwa ndio maana kulikuwa na hali ya ubishi wakashindwa kuelewa. Waliokuwa wanasafiri kwa usafiri mwingine bahati nzuri wao waliwahi lakini sisi kundi la watu 12 nikiwepo mimi tumebaki.”
Wachezaji walioachwa ni Kelvin Yondani, Deogratius Munishi ‘Dida’, Emanuel Martin, Thabani Kamusoko, Donald Ngoma, Haruna Niyonzima, Endrew Vicent ‘Dante’ Juma Abdul, Mwinyi Haji, Deus Kaseke, Ben Kakolanya pamoja na Mkwasa mwenyewe.
Mkwasa amethibisha kwamba, tayari wameshabadilisha tiketi na kupata zitakazowafanya wasafiri siku ya Jumatano April 19 na watafika Dar Alhamisi April 20, 2017.
Kwa mujibu wa ratiba ya ligi kuu Tanzania bara, Yanga wanatakiwa kucheza dhidi ya Tanzania Prisons April 22, 2017.
source:shaffihdauda
Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment