Friday, November 11, 2016

WABUNGE KUMUAGA SAMUEL SITTA NDANI YA BUNGE

SPIKA mstaafu wa Bunge, Samuel Sitta (73) leo ataagwa ndani ya Bunge la Tanzania mjini Dodoma kabla ya kusafirishwa kwenda Urambo mkoani Tabora kwa maziko, ikiwa ni historia kwa kiongozi kuagwa ndani ya Bunge hilo.

Jana, Bunge lililazimika kutengua kanuni kuwezesha kumpa heshima za kipekee Sitta aliyekuwa Spika wa Bunge la 10 kuanzia mwaka 2005 hadi 2010 ambaye leo mwili wake utaingizwa ndani ya Ukumbi wa Bunge kuagwa kwa heshima na wabunge ambao baadhi yao alikuwa nao katika Bunge hilo la Tanzania.

Sitta aliyewahi kuwa pia Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, alifariki usiku wa kuamkia Jumatatu katika Hospitali ya Technical University ya mjini Munich, Ujerumani ambako alikuwa amelazwa akitibiwa saratani ya tezi dume. Alizaliwa Desemba 18, 1942 mjini Urambo.

Mwili wa Sitta uliwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Julius Nyerere (JNIA) jana saa tisa alasiri ukitokea nchini Ujerumani ambako alienda kwa matibabu. Ulipokewa na baadhi ya viongozi wa serikali, viongozi wastaafu, viongozi wa vyama vya siasa pamoja wananchi waliofika uwanjani hapo.

Kwa hatua hiyo ya kutengua kanuni, Mkutano wa Tano wa Bunge la 11 utakuwa umetengua kanuni zake kwa mara ya pili; awali kanuni zilitenguliwa juzi Jumanne ili kusitisha shughuli za Bunge baada ya kifo cha Sitta kutangazwa.

Spika wa Bunge, Job Ndugai jana kwa mujibu wa utaratibu na kanuni za Bunge, alimuomba Waziri, Ofisi ya Rais, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama kutengua kanuni ili kuruhusu shughuli za kumuaga Sitta zifanyike ndani ya Ukumbi wa Bunge kwa heshima ya kiongozi huyo.

“Nitaomba Waziri wa Nchi asimame ili kutengua baadhi ya kanuni ili haya yawezekane,” alisema Ndugai baada ya kuwaeleza wabunge kitakachofanyika leo. Jenista alisimama na kabla ya kutengua kanuni alisema hatua hiyo inafanyika ili kuruhusu shughuli za leo zifanyike kwa matakwa ya kikanuni. “Kwa kuwa Bunge limepata msiba na kwa kuwa Bunge limepanga kumuenzi na kumuaga katika ukumbi wa Bunge, kuna kanuni zitapaswa kutenguliwa,” alisema Jenista.

Kanuni zilizotenguliwa ni ya 139 (1) inayohusu wageni wanaoingia Ukumbi wa Bunge kwamba wataketi maeneo maalumu ya wageni na si katika ukumbi wenyewe na kanuni ya 143 (e)-(f) kuhusu mpangilio wa Bunge wa kukaa, uliowekwa kwa namna ya baadhi ya watu.

“Kanuni hizo zitenguliwe ili kuruhusu ndugu wa karibu wasiozidi 12 waingie kushiriki tukio hilo na kuhusu kanuni ya 143 mpangilio wa ukaaji bungeni utenguliwe ili jeneza liingizwe ndani ya ukumbi na kuwekwa sehemu iliyoandaliwa mbele,” alitoa hoja na wabunge wote kuiunga mkono.



Source:mtembezi

Jiunge na hatukwamii.blogspot.com/ sasa

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia FacebookTwitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video






0 comments:

Post a Comment