Friday, October 7, 2016

WANAFUNZI WA SHULE ZA MSINGI KUANZA KUSAJILIWA KIELETRONIKI

BARAZA la Mitihani Tanzania (Necta) limeunda mfumo wa kutunza taarifa za wanafunzi wa Shule za Msingi (PReM), ambao utasaidia katika uandikishaji wa wanafunzi wote na kupewa namba maalumu, ambayo itamtambulisha mwanafunzi katika ngazi mbalimbali za mafunzo na hivyo kuondoa tatizo la wanafunzi hewa.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, jijini Dar es Salaam kuhusu mafanikio ya baraza hilo, Ofisa Habari wa Necta, John Nchimbi alisema mfumo huo pia utasaidia katika uhamisho wa mwanafunzi kutoka shule moja hadi nyingine ndani ya mkoa au nje ya mkoa.


Alisema mfumo huo utarahisisha utaratibu unaotumika sasa wa kuhamisha mwanafunzi kutoka shule moja hadi nyingine na kuweza kuondoa tatizo la wanafunzi hewa na pia utasaidia katika uandaaji na utoaji wa takwimu za wanafunzi katika ngazi ya shule, wilaya, mkoa hadi ngazi ya Kitaifa.

Aidha, alisema mfumo huo utasaidia katika ufuatiliaji wa taarifa za matokeo ya kila mwanafunzi ili kuhakikisha wadau mbalimbali wa elimu wanapata ufahamu wa kutosha kuhusu ufundishaji na ujifunzaji katika ngazi ya shule.

Alisema baraza limeanza kufanya majaribio ya mfumo huo katika mikoa miwili ya Mwanza na Ruvuma na ifikapo Desemba mfumo huo utaimarishwa ili Januari hadi Mei mwaka 2017, utumiwe na mikoa yote kusajili wanafunzi wa shule za msingi.

“Mfumo huu utadhibiti sana udanganyifu kwa sababu kila mwanafunzi anapoanza shule atapatiwa namba ambayo ataendelea nayo hiyo hiyo katika elimu ya sekondari kidato cha nne hadi cha sita…mfumo huu utakuwa na picha hivyo kudhibiti udanganyifu,” alisema.



Jiunge na hatukwamii.blogspot.com/ sasa

Usipitwe!! Jiunge nasi kupitia FacebookTwitter na Instagram ili kupata habari zote za town! Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video 

0 comments:

Post a Comment