Tuesday, May 23, 2017

Wabunge wadai bila kilimo hakuna Tanzania ya viwanda

WABUNGE wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wamesema bila kuwekeza katika kilimo, azima ya Tanzania kuwa nchi ya viwanda haitatimia.

Kadhalika, wameipongeza Serikali kwa kuondoa tozo 108 zilizokuwa kero kwa wakulima na kuitaka Serikali kuhakikisha tozo zilizoondolewa zinawanufaisha zaidi wakulima na Watanzania, badala ya kuwanufaisha wafanyabiashara pekee. Waliyasema hayo jana kwa nyakati tofauti bungeni Dodoma wakati wakichangia mjadala wa kupitisha makadirio ya mapato na matumizi ya bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ya Mwaka wa Fedha 2017/18.
Mbunge wa Viti Maalum, Mariam Ditopile (CCM), alisema kama Tanzania inataka kuwa ya viwanda, haina budi kuwekeza katika utafiti kwa ajili ya sekta ya kilimo ili kubaini namna bora zaidi za kutumia rasilimali na fursa zilizopo ili kuimarisha kilimo na hivyo kusaidia kufikia haraka azima ya kujenga Tanzania ya viwanda. Alisema tayari fursa za kuinua kilimo na kukifanya uti wa mgongo nchini zimeanza kuonekana kwani kwa sasa Tanzania ndiyo inayouza vyakula na bidhaa za biashara katika nchi mbalimbali duniani zikiwemo nchi za Sudan, Kenya na Uganda wanaonunua mazao ya chakula kama mahindi.
“Nchi kama India inanunua kwetu korosho, choroko na tumbaku. Kwa sasa mipango ni kuipeleka nchi kwenye viwanda ni wakati muafaka wa kuwekeza kwenye kilimo kwa kufanya utafiti za kisayansi za namna bora ya kuendeleza kilimo chetu kwa sababu kilimo ndio ajira, chakula na fedha,” alisisitiza. Alisema Tanzania inasifika kwa kufanya utafiti, lakini pamoja na kuwa na uwezo huo bado haujatumika vizuri kuendeleza mambo ya msingi yakiwamo maeneo ya kilimo, mifugo na uvuvi.
“Kwa mfano sisi ndio wenye eneo kubwa katika Ziwa Victoria, lakini takwimu za kidunia zinaonesha Uganda yenye sehemu ndogo katika ziwa hilo ndiyo inayoshika nafasi ya juu; ya sita duniani kwa uvuvi huku sisi Tanzania tukishika nafasi ya nane,” alisema. Mbunge wa Mbinga Mjini, Sixtus Mapunda (CCM) aliitaka serikali iwekeze kwenye utafiti wa kilimo ili kuyabaini maeneo ya kijiografia na kisayansi yanayoweza kuikuza kwa kasi sekta hiyo ya kilimo inayokwenda sambamba na sekta ya viwanda.
“Kwa mfano Morogoro ina udongo wenye rutuba na mito inayotiririsha maji kwa mwaka mzima, utafiti ukifanyika wa namna bora ya kutumia rasilimali hizo, ni wazi kuwa Morogoro pekee inaweza kulisha Tanzania nzima,” alisema. Pamoja na hayo mbunge huyo alisema si kweli utitiri wa kodi zilizofutwa na serikali umewalenga zaidi wafanyabiashara na wenye kampuni na si wakulima kwa kuwa wafanyabiashara na kampuni hizo kutokana na kufutwa kwa tozo hizo kuanzia sasa watanunua mazao na bidhaa hiyo kwa bei inayostahili.

source:habarileo
Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment