Monday, April 3, 2017

MJANE ADHULUMIWA NYUMBA ALIOACHIWA NA MUMEWE, AIOMBA SERIKALI KUMSAIDIA KUPATA HAKI YAKE

Mjane Farida Saleh Amrani (Pichani juu) amejitokeza mbele ya vyombo vya habari na kulalamika kudhulumiwa nyumba yake aliyoachiwa na marehemu mme wake aliyefariki mwaka 2011.
Akizungumza wanahabari huku akionyesha hati halali za nyumba hiyo yenye kitalu namba 2111 iliyopo Mbezi Beach Kata ya Maliasili, Farida alisema kuwa katika nyumba hiyo walihamia mwaka 2002 na hati ya nyumba hiyo ilikuwa kwa mwanasheria kipindi chote hata pale marehemu mumewe alipofariki.
Amesema kuwa, baada ya mume wake kufariki mtoto wa marehemu mkubwa aliambiwa afungue mirathi lakini akawa anasema taratibu za kabila la kihaya ni baada ya mwaka mmoja kumalizika.
Farida ameeleza kuwa, mumewe Alfred Kyoma alifariki akiwa safarini Bukoba na amemuacha na watoto wawili ambao baada ya kumalizika kwa msiba familia nzima walikubaliana nyumba ipangishwe ili fedha zitakazopatikana ziwasomeshee watoto ambao mmoja yupo kidato cha tano sasa hivi na mwingine cha kwanza.
Nyumba hiyo kwa mujibu wa nyaraka za manunuzi inaonyesha kununuliwa na Yusuph Shaban Omari Mkazi wa Dar es Salaam  huku ikionyesha kuwa ameuziwa na kaka wa marehemu lakini katika hati ya mauzo ikiandikwa Alfred Athanas Kyoma akishirikiana na mtoto wa Marehemu.
Wanahabari walishuhudia nyumba hiyo ikiwa imefungwa kwa ndani huku kukiwa na kampuni ya Ulinzi binafsi ikiendelea kulida nyumba hiyo ambapo taarifa za awali zinaeleza kuwa, Mpangaji aliyepangishwa ili pesa ziweze kusomeshea watoto wa marehemu, aliondolewa vitu vyake nje ya nyumba hiyo na kisha kuwekwa mlinzi huyo.
Kwa upande wao, Majirani wa nyumba hiyo Wamesema kuwa siku chache zilizopita waliona watu wakivunja nyumba na kuingia ndani na kutoa vitu ndani vya mpangaji anayekaa hapo ambaye alikuwa amesafiri.
“Tulishangazwa na kitendo hiki maana hakikuwa cha kiungwana. Na tulipowasiliana na Mama mwenye nyumba naye hakua na taarifa ndio kama unavyoona. hadi sasa panalindwa hakuna mtu anayeingia humo ndani” alieleza  Mjumbe wa Shina la nyumba 10, Bi Eline Kashumba ambaye pia ni jirani huku akieleza kuwa taratibu za kuwatoa wapangaji ndani ya nyumba hiyo na zile za mauzo yeye kama mjumbe hakushirikishwa na zaidi aliwatupia lawama Mwenyekiti na Mtendaji wa Serikali za Mitaa wa mtaa huo.
Kwa sasa nyumba hiyo imewekwa mlinzi huku Mama mwenye yumba hiyo ambaye ni Mjane jitihada za kumwambia afungue mlango wa geti hilo ziligonga mwamba  na kuishia kuzungumzia nje ya nyumba hiyo ambapo ameiomba Serikali kuingilia kati suala hilo kwani kuna ubabaishaji kwani waliofanya tukio hilo wamefoji nyaraka za nyumba hiyo kwa kushirikiana na Kigogo mmoja wa Serikali katika Wizara ya Ardhi.
“Nyumba hii tumejenga mimi na mume wangu. Na majirani wote wapo na ni mke halali na mume wangu amefariki nashangaa shemeji yangu ananigeuka kwa kushirikiana na mtoto mkubwa.  Wameuza nyumba hii kwa kiasi cha shilingi milioni Sitini (60) thamani ambayo hata kiwanja huku Mbezi hupati. Naiomba Serikali kuliangalia hili kwani huu ni wizi na utapeli nataka mamlaka kumchunguza huyu aliyenunua hii nyumba” alimalizia Mama huyo.
Nyumba hiyo inavyoonekana 
Mjane Farida Saleh Amrani akionesha baadhi ya hati halisi alizoachiwa na mumewe kumili nyumba hiyo akionyesha kwa waandishi wa Habari (Hawapo pichani).
Baadhi ya majirani ambao pia wanajumuiya na Mama Mjane huyo wakitoa ushuhuda kwa waandishi wa habari (Hawapo pichani) wakati wa tukio.
Baadhi ya majirani ambao pia wanajumuiya na Mama Mjane huyo wakitoa ushuhuda kwa waandishi wa habari (Hawapo pichani) wakati wa tukio.
Sehemu ya ukuta wa nje wa nyumba hiyo inavyoonekana


Source:dewjiblog
Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment