Tuesday, April 18, 2017

Mchungaji Rwakatare atoa ya moyoni kuteuliwa Mbunge Viti Maalum

Mbunge wa Viti Maalum na Mchungaji  Kiongozi wa Kanisa la Mlima wa Moto lililopo Mikocheni B, Assembles of God, Dkt. Getrude Rwakatare, amemshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa kumkumbuka na kumteua katika nafasi ya ubunge wa Viti Maalumu.

Dkt. Rwakatale ametoa shukrani  hizo Jijini Dar es Salaam katika ibada kanisani kwake na kusema kuwa uamuzi huo ni kutokana na Mungu kumuona.

“Nina furaha ya mwili na roho kwa sababu Yesu amefufuka na pia Mungu amenirudisha bungeni, Mungu amejibu maombi yetu, tulifunga siku tatu na ile ya mwisho akajibu,”  amesema Mchungaji Rwakatare.

Amesema ana kila sababu ya kumshukuru Rais Dkt. Magufuli kwa sababu  wapo wanawake wengi ambao angeweza kuwachagua na kuwapa nafasi hiyo.

“Nakishukuru pia Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa kunikumbuka, wapo wanawake wangapi lakini leo mlima wa moto katikati ya maombi, Mungu ametenda,” ameongeza Mchungaji Rwakatare.

Aidha, Dkt. Rwakatare alitumia ibada hiyo kuwaomba msamaha watu aliowakosea huku akiwasihi waungane naye kumshukuru Mungu katika maombi.

“Katika Luka 24:1-9 tunasoma habari kuhusu ufufuko wa Yesu, tumezoea makaburini huwa kuna habari mbaya lakini kwa Yesu ilikuwa tofauti, ilikuja habari njema. Alitangaza msamaha hata alipokuwa msalabani basi naomba mnisamehe nilipokosea maana na mimi ni mwanadamu,” amesema.

Aprili 14, mwaka huu Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kupitia kwa Mkurugenzi wa tume hiyo, Ramadhan Kailima ilitangaza jina la Mchungaji Rwakatare kuwa mbunge baada ya Chama cha Mapinduzi (CCM) kupeleka jina lake.


Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment