Tuesday, April 18, 2017

Bunge kujadili hali ya mauaji inayoendelea nchini

Mbunge wa Bukombe, Mhe. Dotto Biteko ametoa hoja ya kuahirishwa kwa shughuli za bunge ili Bunge liweze kujadili hali ya mauaji inayoendelea nchini ikiwemo mauaji ya askari polisi waliouawa na watu wanaotuhumiwa kuwa ni majambazi katika eneo la Jaribu Mpakani, Wilaya ya Kibiti Mkoani Pwani. Hoja hiyo imeungwa mkono na wabunge kadhaa wakiwemo Cosato Chumi (Mafinga Mjini) na Amina Mollel (Viti Maalum)

Akitolea ufafanuzi hoja hiyo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe Mwigulu Nchemba amesema serikali inachukulia jambo hilo kwa ukubwa na uzito mkubwa.
“Kama ilivyotolewa kauli na Waziri Mkuu serikali inalichukulia mambo haya kwa uzito mkubwa na inawahakikishia wananchi
matukio ya uhalifu yaliyotokea ndio yametupa chachu zaidi ya kupambana na matukio kama haya na pia tunawaomba wananchi watoe taarifa na wala wasiogope maana tuna mfumo bora sana wa kuwalinda watoa taarifa wote” Ameeleza Waziri Nchemba ambaye pia ametoa pole kwa familia za askari wote waliopoteza maisha wakiwa katika kazi ya kulinda wananchi na amani ya nchi.

Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe Job Ndugai, amelieleza Bunge kwa kuwa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya Mwenyekiti wake Balozi Adad Rajabu itakutana leo na mawaziri husika ili kupokea taarifa ya mambo haya ni vyema Bunge likatoa nafasi kwa kamati hiyo kukutana kwanza na kupokea taarifa hiyo.


Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment