Wednesday, June 7, 2017

RC Mghwira: Mimi sio mpinzani wa maendeleo

MKUU mpya wa Mkoa wa Kilimanajaro, Anna Mghwira, amemhakikisha Rais John Magufuli na Watanzania kwa jumla kuwa katu yeye sio mpinzani katika masuala yanayohusu maendeleo na maslahi ya taifa.
Aliyasema hayo jana Ikulu katika hafla ya kuapa mbele ya Rais Magufuli kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro baada ya Rais kumteua hivi karibuni kuziba nafasi ya Said Meck Sadick aliyemwomba Rais kujiuzulu akisisitiza kuwa, changamoto za kiafya alizo nazo hazitamwezesha kuendana na kasi ya maendeleo katika Serikali ya Awamu ya Tano.
Mghwira alisema anavyofahamu yeye ni kwamba, kazi za mkuu wa mkoa ni kusimamia shughuli za maendeleo kwenye mkoa na akaongeza kuwa, hakuna chama kinachopinga maendeleo ya kila eneo la nchi na nje ya mipaka ya nchi.
“Nimesema hii ni heshima kwa taifa letu, ni heshima kwa umoja wa nchi yetu, na ni heshima kwa siasa za umoja wa nchi yetu… Kumekuwa na minong’ono mingi sana kuwa Rais analeta nini; kuteua watu wanaoitwa wapinzani, mimi sio mpinzani wa maendeleo,” alisema Mghwira.
Katika hafla hiyo, Rais Magufuli alimtaka aende akachape kazi ili kuwaondolea kero wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro, licha ya kuwapo baadhi ya watu watakaomsema na kumbeza kwa kumwonea wivu.
Rais alisema alimchunguza Mghwira na kujiridhisha kuwa ana uwezo wa kuwatumikia wananchi wote bila tatizo. Alisema ingawa wapo wanasiasa wengi kutoka vyama vya upinzani wanaomwomba awateue kwenye nyadhifa mbalimbali serikalini, amekuwa akiwakatalia kwa vile anataka upinzani uendelee kuwepo nchini.
Katika hafla hiyo, Rais Magufuli alisema hawezi kuteua watu wanaosema sema ovyo, bali anateua mtu anayejua na kuamini kwa dhati kuwa, akimpeleka sehemu atafanya kazi kwa niaba ya Watanzania wote.
Alisema anajua kitendo cha kumteua Mghwira katika wadhifa huo kitazua maneno mengi kutoka kwa wana CCM na wanachama wa vyama vya upinzani kutokana na sababu mbalimbali hasi ukiwamo wivu, lakini akamtia moyo kuwa astahimili yote kwa kuwa hawezi kuepuka kusemwa.
Rais alisisitiza kuwa, yeye hateui watu wa hivi hivi, bali huwachunguza hadi kuridhika na uwezo na umakini alio nao mtu. “Kusemwa utasemwa tu, umeshaingia humu wengine watakuonea wivu, wapo watakaokuonea wivu wa kwenye chama chako, wapo wana CCM watakaokuonea wivu kwa sababu walitaka nichague tu kutoka CCM.”
“Wapo watakaokuonea wivu kutoka Chadema kwa sababu sikuchagua kutoka huko, pamoja na kwamba wako wengi wanaoniombaomba; mpaka wabunge, lakini nimesema hapana, nataka upinzani uwepo,” alisema Rais Magufuli.
Akaongeza, “Wapo watu kila kitu ni kupinga tu, mimi siteui watu wanaopiga piga kelele, nateua mtu ambaye najua nikimpeleka mahali atafanya kazi kwa niaba ya Watanzania, nenda ukafanye kazi, katumikie Watanzania, kamtangulize Mungu, kafanye kazi kwa niaba ya Watanzania,” alisema Mafuguli baada ya kumwapisha Mghwira.



Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment