Friday, June 23, 2017

Marufuku wajawazito kurejea shuleni

RAIS John Magufuli (pichani) amepiga marufuku mpango unaopigiwa debe na asasi ziziso za kiserikali wa kutaka mwanafunzi anayejifungua kurudi shule, kwa maelezo kuwa mpango huo ni laana. Amesisitiza kuwa kamwe katika kipindi cha uongozi wake, hataruhusu jambo hilo.

Akizungumza jana wakati wa kufungua barabara ya Bagamoyo – Msata, Rais Magufuli alisema serikali yake haiko tayari kutoa Sh bilioni 18.77 kila mwezi kwa ajili ya kusomesha wazazi. Badala yake, alisema serikali inatoa fedha hizo kwa ajili ya wanafunzi wa shule za msingi hadi sekondari wasome bure.
“Tukienda kwa mzaha wa namna hii, tutafika pabaya, mtu amezaa kwa raha zake, mnataka arudi shuleni akiwa na mtoto si atawafundisha wengine! Mnataka akipata mtoto wa kwanza akinyonyesha arudi shuleni, akipata wa pili arudi, akipata wa tatu arudishwe shule, yaani mnataka tusomeshe wazazi?” alihoji Rais Magufuli.
Alisisitiza kuwa hakuna mwenye ujauzito au mtoto, ambaye ataruhusiwa kurudi shuleni katika kipindi cha utawala wake. “Akae nyumbani alee vizuri mtoto wake maana amechagua njia hiyo… tukiruhusu tutawafanya wanafunzi wengine wazae kwa wingi maana mchezo ule ni mtamu na kila mtu atapenda aufanye… chini ya utawala wangu nasema hapana,” alieleza Dk Magufuli kwa sauti ya ukali na msisitizo.
Aliagiza vyombo vya dola kwamba wakati msichana atabaki nyumbani kulea mtoto, wale wanaohusika kuwapa mimba wanafunzi hao, wakafungwe miaka 30 ili nguvu alizotumia kumpa ujazito, akazitumie kuzalisha mali akiwa gerezani.
“Akitoka jela nguvu atakuwa hana tena na yawezekana akakomea mtoto huyo huyo mmoja,” alisema Rais Magufuli ambaye alitoa mwito kwa NGO ambazo zinatetea jambo hilo, zikafungue shule malumu kwa ajili ya wasichana ambao wamejifungua.
Katika suala hilo, Rais alisisitiza kuwa hata kama ni mtoto wake akipata ujauzito akiwa shule, kamwe hawezi kurudi shule. Alizitahadharisha NGO kuwa makini na kunakili mambo ya kigeni kwamba watanakili na mambo ya ajabu yakiwemo ya ushoga, licha ya kuwa wafadhili wa mambo hayo wanakuja na misaada.
“Wakati mwingine tunapata laana za ajabu kwa kufanya mambo yasiyostahili,” alisema Rais Magufuli. Ageukia ufisadi wa pembejeo Rais Magufuli alisema kwa sasa anajiandaa kuchukua hatua kwa mafisadi, ambao walitumia vibaya fedha za pembejeo kwa kuandikisha watu ambao tayari walishakufa ili mradi waibe fedha hizo.
Dk Magufuli alisema anajua miongoni mwa watu waliofanya ufisadi wa fedha za pembejeo, kuna viongozi wa wilaya na mikoa na aliagiza viongozi wa mikoa, kuhakikisha wanawaweka hadharani wale wote ambao walifisadi fedha hizo.
“Mtu anaandikisha maiti, sijui walikuwa wanatoka huko kaburini kuja kuchukua pembejeo, nafanya haya kama kuna sehemu Watanzania tumekosea basi tukatubu dhambi zetu,” alisema Rais Magufuli.

source:habarileo
Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment