Wednesday, June 21, 2017

JPM: Wameanza kunyooka

RAIS John Magufuli amesema anawachukia wezi wa rasilimali za nchi na kwamba tayari amekwishawanyoosha baadhi yao na anaendelea kuwakomesha wengine, kwa sababu ndio walioliingiza taifa katika umasikini.
Aidha, Rais amesema katika kuhakikisha kunakuwa na umeme wa kutosha kuendesha nchi ya viwanda, serikali itajenga bwawa kubwa la kuzalisha nishati hiyo katika maporomoko ya maji ya Stieglers Gorge yaliyoko kwenye Mto Rufiji ndani ya Pori la Akiba la Selous.

Alisema hayo jana katika viwanja vya Bwawani wilayani Kibaha mkoani Pwani akiwa katika siku yake ya kwanza ya ziara ya kikazi ya siku tatu, iliyolenga kuzindua viwanda vitano pamoja na kuzungumza na wananchi. Alisema Mungu hakuwaletea Watanzania umasikini kwa sababu ni nchi yao, ina rasilimali nyingi yakiwemo madini na vivutio vinavyoifanya ionekane ni tajiri.
Hata hivyo, alisema watu wake wanaishi katika hali ya umasikini kutokana na wizi wa wachache wasio waaminifu, wakiwemo baadhi ya watumishi walioaminiwa na umma, lakini wakageuka na kusaliti taifa. Aliwaomba Watanzania kumwombea kwa kuwa ameasisi vita ngumu itakayoumiza wachache, ili kunufaisha wengi. “Watanzania niombeeni kwa kuwa nimeanzisha vita itakayoumiza wachache ili wengi wanufaike.
Hii ni vita kwa sababu itaumiza baadhi ya watu. Niombeeni kwa Mungu niishinde kwa faida yetu sote. Nachukia wezi na nitalala nao sambamba mpaka wakome na waione dunia ilivyo kwa kuwa wametufanya maskini,” alisema. Akaongeza, “Mimi nachukia wezi, na kwa kweli wezi watakoma tu, awe mwizi wa Tanzania, awe mwizi wa Ulaya, awe anatoka Magharibi, Mashariki, Kaskazini au Kusini, mwizi ni mwizi tu.”
Rais alisisitiza kuwa, baadhi ya watu walioliingiza Taifa katika umaskini kwa makusudi, ameanza kuwashughulikia na wengine wameanza kunyooka. Aliwatahadharisha waliopo serikalini kufanya kazi kiuadilifu ili wasiwepo wanaoendelea kulisababishia taifa upotevu wa rasilimali akisema, hatawaacha waendelee kuliibia taifa, kwa sababu alichaguliwa na Watanzania ili atetee maslahi ya wote, wakiwemo wanyonge.
Alizungumzia ujenzi wa bwawa la kuzalisha umeme na kusema kuwa pamoja na kupanua mradi wa umeme wa Kinyerezi 1, 2 na 3 ili nchi iwe na nishati hiyo ya kutosha, watawatumia wataalamu waliojenga bwawa kubwa la kuzalisha umeme Ethiopia ili wajenga kama hilo nchini. Asifu uongozi Pwani Rais alionesha kufurahishwa na uongozi wote wa Mkoa wa Pwani kuanzia Mkuu wa Mkoa hadi ngazi za chini kwa jitihada uliozionesha kuhakikisha uanzishaji wa viwanda unashika kasi, huku vingine vikikamilika tayari kwa kuzinduliwa na vingine vikiwa katika hatua mbalimbali za maendeleo.

source:habarileo
Tuandikie Maoni Yako Hapa Chini. Usikose kujiunga naYoutube kuangalia video za kufurahisha na kuvunja mbavu.

0 comments:

Post a Comment